Hinweis: Um die korrekte Darstellung der Seite zu erhalten, müssen Sie beim Drucken die Hintergrundgrafiken erlauben.
Slider Bild - CC BY-NC-ND 4.0
Slider Bild - CC BY-NC-ND 4.0
Slider Bild - CC BY-NC-ND 4.0
1/3

Mtemba, Bomba la tumbaku

Sammlung Braun
r 2018 / 18555 a
Taasisi inayotoa
Museen Stade
Eneo la Mkusanyiko
Sammlung Braun
Nambari ya uvumbuzi
r 2018 / 18555 a
Kichwa
Mtemba, Bomba la tumbaku
Nyenzo
Mbao,
Ton
Kiungo cha dondoo
https://www.amani-stade.gbv.de/item/sw_ms_a6cf54c5-61ad-4a3c-a360-e6637fb069b1
nakala kwenye ubao wa kunakili
Kikundi cha kitu / kitu cha mtu binafsi
Kitu cha mtu binafsi
Uainishaji
Vyombo vya kuvuta sigara  
Uzalishaji
Wakati
mpaka ca. 1905-03-11
Mtu
  • Person (Mtengenezaji)
Mahali
  • Tansania
Ethnolojia
  • Shambaa  
Kununua / Uuzaji
Wakati
1905-03-11
Maelezo
"Jumamozi 24. Nimepokea Kiko cha Waschambaa. Kichwa cha udongo na mrija wenye urefu wa[...] [?] 30 cm. (= 12 pesa). [mchoro ya] [...]" [Utafsiri]

chanzo: Museum der Kulturen Basel, VI 56197, 44 (80)
mwandishi: Karl Braun
Mtu
  • Mtu, haijulikani (Mchuuzi)
  • Braun, Karl (* 1870 † 1935) (Mnunuzi)
    GND Explorer
Mahali
  • Amani
Malipo
Wakati
kutoka 1905-03-11
Maelezo
"24. Kiko cha Schambala / udongo mweusi, 30 cm kijipaipu kirefu kutoka mabao uliotobelewa (waya unaowaka). (= pesa 12 ) / Amani 11 mwezi wa tatu 1905 / TB. 44,80 [mchoro]" [Utafsiri]

chanzo: Museen Stade, r 2018 / 18566
mwandishi: Karl Braun
Mtu
Nambari za hesabu za zamani
  • 24
Urithi
Wakati
1934-07-17
Maelezo
Mnamo mwaka 1934, aliyekuwa mkurugenzi wa Taasisi ya Biolojia ya Kilimo na Misitu (Biologische Reichsanstalt für Land- und Forstwirtschaft) Karl Braun (1870–1935) alitoa kile kinachoitwa “Kolonialsammlung Braun” (Makusanyo ya Mkoloni Braun) kwa Jiji la Hanseatic la Stade, au tuseme aliyekuwa mwakilishi wake, meya wa wakati huo Hans Arthur Meyer (1884–1961). Tazama faili „Uhamisho wa makusanyo ya kikoloni kutoka kwa diwani mkuu wa serikali Profesa Dk. Karl Braun huko katika Jiji la Stade” („Überlassung einer Kolonialsammlung vom Oberregierungsrat Professor Dr. Karl Braun in Stade an die Stadt Stade") katika Jimbo la Saxony ya Chini Hifadhi ya Nyalaka ya Stade (Niedersächsischen Landesarchiv Standort Stade).

chanzo: Niedersächsisches Landesarchiv Standort Stade, Dep. 10 Nr. 03025
Mtu
  • Braun, Karl (* 1870 † 1935) (Mfadhili)
    GND Explorer
  • Hansestadt Stade (Mpokeaji)
  • Hans Arthur Meyer (1884 - 1961) (Mpokeaji)
Mahali
  • Stade
Mkopo
Wakati
1997-02-17
Maelezo
Mnamo mwaka 1997, aliyekuwa mtunza kumbukumbu wa jiji kwa wakati huo Jürgen Bohmbach anahitimisha makubaliano ya makabidhiano kwa mkopo wa kudumu katika Jumba la Makumbusho (Museumsverein Stade e.V.) chini ya aliyekuwa mkurugenzi wa wakati huo Gerd Mettjes kwa kutia saini. Baadaye, makusanyiko kutoka kwa Karl Braun yalihamishiwa kwenye Jumba la Makumbusho (Museumsverein Stade e.V.) kwa ajili ya utunzaji.

chanzo: Museen Stade, Vereinbarung Leihgabe "Brauns'sche Kolonialsammlung"
Mtu
Mahali
  • Stade
Scientific use:
Wakati
2023-06-09
Maelezo
I: Basi naomba nikupe picha ambayo imesajiliwa kwa namba 2018_18555_001 hebu angalia unaweza ukafahamu hicho ni kitu gani? R: Hiki nakitambua I: Ni nini hiyo? R: Huu mtemba huu I: Mtemba? R: Eeeeh I: Hahahhah R: Wanaita Kiko I: Kiko? R: Eeeeh I: Ahaah R: Kisambaa ni Kiko I: Kisambaa ni kiko? R: Eeeeh kiko I: Mtemba ni kilugha gani? R: Tuseme inachanganya mataifa ya makabila mengi lakini katika lugha inayoeleweka ni mtemba I: Mtemba ni kisambaa au kwa wote? R: Ni kama Kiswahili I: Kiswahili R: Eeeeeh I: Ni watu wa makabila gani hasa wanatumia mtemba? R: Wasambaa, hata baadhi ya makabila ya bara wako wanaotumia mtemba I: Makabila gani hayo ya bara? R: Watu wa tabora, shinyanga ukienda mikoa ya huku mbeya, iringa huko watu wanatumia mitemba I: Kifaa hicho kinatumikaje unaweza ukatuambia? R: Hiki wanatumia mtu anachukua tumbaku yake kule shambani akija hapa anaikata kata vidogo vidogo anaweka hapo anaweka na moto wake hapo juu inashika basi anavuta kwa kutumia mtemba huo I: Anavuta? R: Eeeeeh ndiyo nilivoona mimi hata kwa mababu zetu eeeh I: Ni watu gani wanatumia sana mtemba kwa kijinsia? R: Sanasana jinsia ya kiume I: Ya kiume? R: Ndiyo I: Wa umri gani? R: Umri sasa kwasababu hivi vimepotea matumizi yake ni agahalabu sana kumkuta mtu lakini ile miaka kuanzia 50 huko kwenda mbele I: Walikuwa wanatumia mtemba? R: Sana eeh I: Kwanini walikua wanatumia wazee wa miaka 50 kwenda mbele? R: Unajua wakati huo ukiona mtemba unavutwa sanasana makabila hawa wenyeji mambo ya sigara hii ya kiwandani walikuwa hawatumii alikuwa na shamba lake ana miti yake hapo nje ya tumbaku anakausha majani yake au lile la kutwanga lile linatwangwa linafanyiwa lina kama falima yake lina minywa lile linaanikwa likikauka imekaa ina round hivi ikikauka anachukua kale kamoja anafinyanga, finyanga kwenye kiganja hivi anatengeneza anatumbukiza kwenye mtemba wake anawasha moto wake anavuta I: Anavuta? R: Eeeeh zilikuwa za aina mbili kuna ile ya majani ya kukata kata na kuna ile wanatumia majani mabichi yale wanayatia kwenye kinu wanaya twanga yakiwa tayari kitu kama faluma fulani wanaweka hapa anakandamiza anaanika yakikauka anabendua kidogo anaweka ana nanii anatia ule uvumbi wake anaeka kwenye mtemba wake hapa ndiyo anavuta eeh viko vya aina mbili tofauti I: Viko vya aina mbili? R: Eeeeh hayo ndiyo yalikuwa matumizi ya tumbaku hayo I: Kifaa hiko bado kinatumika au kimepotea sasa? R: Kwa wastani saivi unakiona kwa bahati sana labda hivi vya wavulana vya kulegesha tu ila kuvikuta dukani utavikuta ila siyo mara nyingi sana I: Unadhani inaweza ikafika wakati mtemba ukawa hautumiki tena? R: Itafikia huko kwenye miaka ya mbeleni I: Kitu gani kitapelekea mtemba usitumike tena? R: Unajua hizi hapa za asili zilikuwa hazina madhara sana uvutaji wa asili maana yake nimeona kuna baadhi ya watu mpaka unamkuta anavuta hata kukohoa hakohoi kwasababu havuti hizi za viwandani anavuta hizi za kienyeji mtu unamkuta hadi leo anavuta lakini unakuta huyu aliyeanza baada ya miaka mingapi unamsikia anakohoa tena either akaambiwa acha kuvuta lakini hizi za asili zilikuwa kwa kweli mimi nilivoona huko mwanzoni humkuti mtu anakohoa hovyohovyo akitumia hiyo I: Kwahiyo unadhani kitu gani kitapelekea isiendelee kutumika kwa sasa kwa mawazo yako mzee [anonymous]? R: Hii mtemba I: Eeeeh R: Watu wanabadilika I: Wanabadilika vipi? R: Wanabadilika kufuata haya mambo ya kileo kuliko unakwenda ugenini una limtemba kama hili unakaa kwa wenzako wanakuangalia huyu nae anafanya nini ila akitia mfukoni anatoa sigara yake akiwasha hapa moshi wake ukienda hivi anaupenda eeh hauna harufu kama ile inayotoka huku pale mwanzoni zamani kulikuwa kuna tumbaku special imetengenezwa kutoka huko huko ukitia kwenye mtemba wako hapa ukiwasha kila mtu anapenda ile harufu yake ilikuwa ni nzuri sana I: Eeeh R: Sasa siku hizi hailetwi ile hatuioni huku ndiyo utakuta watu wengi wamehamia kwenye sigara hizi sm, sports kwamfano ukiangalia sanasana sigara kali hizi hapa unaona kwa mara chache sana sigara kali lakini hizi zenye filter hizi ndiyo nyingi wanavuta watu za mitemba hizi hapa huko tunapokwenda itakua ni aghalabu I: Kwasababu ya ujio wa usasa? R: Eheeeh! I: Sawasawa na ili mtemba utumike ulikuwa unahitaji kitu gani kingine kinatakiwa kiendane sambamba? R: Maandalizi ya ile tumbaku yenyewe unajua maandalizi ya kizamani yalikuwa hayafati viwango yani ilivotoka shamba ni hivohivo basi itatumika hivohivo eh I: Kwahiyo mtemba ulikuwa unahitajika uwe na tumbaku? R: Eeeeh tumbaku I: Bila tumbaku huwezi ukatumia mtemba? R: Aaaaa huwezi kutumia I: Kitu gani kingine cha kutumia na mtemba tofauti na tumbaku kama unakijua tuambie mzee [anonymous]? R: Wengine anachukua sigara ile anaifumua ile anaitia kwenye mtemba anawasha anavuta eeeh baadhi ya wengine waokataa za kutoka shambani moja kwa moja anachukua sigara anaifungua karatasi ile yenyewe anaitumbukiza kwenye mtemba wake anawasha basi anakuwa anaendelea kuvuta I: Kwa makabila yaliyotajwa wanaotumia mtemba unadhani utamaduni wa kutumia mtemba kwa wao utaondoka na huo usasa ulio usema? R: Polepole utasogea kwasababu hata zamani mtu alikuwa yani hata ugali unaotoka mashine hali anataka ugali wa kutwanga kwenye kinu lakini japo utakaa mahali kutwa nzima hutasikia mtwangio hata saa hii wote wako kwenye ugali wa mashine kwahiyo hata hiyo itafika wakati wake utaondoka tu I: Sawasawa na ilikuwa na umuhimu gani mtemba? R: Mtemba kwasababu mimi sikuvuta ila hao wenyewe wavutaji walikuwa wanaisifia nini huko wenyewe I: Maana kuna watu wanasema ukiwa unatembea na mtemba unaonekana kidogo ni mtu mwenye hadhi fulani tofauti na watu wengine hiyo ilikuwaje? R: Inategemea kweli kama unavoongea kuna baadhi ya sehemu nyingine mtu mzima makamo kama mimi ukitembea bila bakora unaonekana huyu nae vipi bakora, bakora hizi lakini sahivi utakuta katika kundi la watu wengi watu wawili tu ndiyo wenye bakora kwahiyo mambo yanaenda na wakati I: Aaaah R: Ndiyo sasa hata huu mtemba hapa unashuka kiwango I: Na unadhani mtemba bado unatengenezwa kwa mazingira yetu ya sasa na unaweza ukafahamu ni wapi wanatengeneza? R: Wako lakini utakuta siyo maeneo yote ni wachache sana katika mia unaweza ukakuta wawili au mmoja tu I: Kwanini wachache? R: Unajua kama vile kuchekwa na baadhi ya wenzako kwamba we nae bado unatumia hayo mambo ya kizamani hayo saa nyingine kile kitu kinawaingia kwahiyo na wao wanaamua anaacha kutumia I: Kwahiyo inaonekana ni kitu cha kizamani? R: Eeeeh ni kitu cha kizamani eeh I: Hahhhahha sawasawa na umesema waliokuwa wanatumia ni wazee R: Wazee ndiyo I: Wajinsia gani? R: Sanasana wa kiume I: Ya kiume? R: Eeeeh I: Kwanini sanasana walikuwa wazee wakiume? R: Ukikuta jinsia ya kike ni bahati mbaya sana ukute mama anavuta mtemba ni mara chache sana kuona ila sana, sana ilikuwa ni wanaume I: Wanaume? R: Eeeeeh I: Nani watu gani walikuwa wakitengeneza mitemba ni wanawake au wanaume? R: Wanaume I: Wanaume? R: Eeeeeh ndiyo walikuwa wanatengeneza mitemba I: Kwanini walikuwa ni wanaume zaidi? R: Unajua hapo zamani kuna vitu yani kila kitu kilikuwa na jinsia ambayo huyo hata akikutwa anacho hakuna gharama za kuuliza kwamfano hivi hapa mwanaume ukutwe na kinu na makopa unafunda makopa hapo watakwambia huyu naye vipi ni mzima akili yake anafunda makopa kweli I: Hahahhahha R: Kwamba kila kitu kilikuwa kina wenyewe jinsia ya kike walikuwa na vitu vyao na jinsia ya kiume pia I: Sawasawa na kwasasa unaweza ukafahamu mikoa umesema ni Dodoma, ni mikoa gani mingine wanatengeneza? R: Sanasana mikoa ya bara I: Ya bara? R: Ndiyo mikoa ya bara eeeh I: Kama? R: Hata mkoa wetu wa Tanga huu kuna baadhi ya kata nyingine kidogo zipo ndani ndani mtu anaweza akakaa wiki au mwezi hajaona gari huko aliko gari anafaa kuzisikia kwa huko zinapita lakini haikuti hapa na hapo sasa unakuta sehemu kama zile baadhi ya haya mambo ya kizamani bado yapo tuchukulie mfano nyumba kuna nyumba ambazo za nyasi au nyumba haina dirishakabisa hivi hapa katika maeneo haya nyumba kama hiyo huwezi ukaikuta lakini kuna baadhi ya sehemu nyumba hizo zipo unazikuta sasa ni sawasawa na huu mtemba zipo sehemu bado utaukuta mtemba na wanavuta kama kawaida eeeh I: Na mtemba unatengenezwa kwa kutumia kitu gani? R: Kulikuwa na vya aina mbili kulikuwa na cha udongo na kuna cha mti I: Cha mti? R: Eeeeh I: Udongo wa aina gani ulikuwa unatumika? R: Udongo wa mfinyazi I: Udongo wa mfinyazi? R: Ndiyo I: Na huo wa mti ni mti gani ulikuwa unatumika kutengeneza? R: Kuna mti fulani lakini mimi siujui jina lake sanasana hiki chungu hiki kinachoshikia, ile tumbaku kile nicha mfinyazi sasa ule mrija wake yani unaotoa moshi kuja kwa wewe unaevuta ni cha mti I: Cha mti? R: Ndiyo I: Kwanini walikuwa wanatumia mfinyazi? R: Kwasababu moto hapa hauunguzi I: Huunguzi? R: Ndiyo na hata kama kimekamilika sawasawa na ulivo kichoma saa nyingine hata ukiangusha hakiwezi kupasuka I: Aaaah R: Ndiyo I: Sawasawa na vifaa vilivokuwa vinatumika kutengenezea Mtemba vilikuwa vikibadilika, badilika kadri ya miaka ilivokuwa inaenda au ilikuwa ni hivohivo? R: Unajua saa nyingine ni ufundi au design ya kile kitu ukute mtu ameona kwa mwenzake huko akija nae huku anataka atoe design, ile ile I: Ndiyo R: Eeeeh I: Material tunazungumzia R: Material ni yale yale lakini sasa ule ufundi ndiyo unatofautiana I: Ndiyo unatofautiana? R: Ndiyo I: Mtemba kama huu ukiuangalia kwenye picha kwa hali yetu ya sasa ukiletwa ukawa unauzwa sokoni unaweza kununuliwa kwa gharama kiasi gani au utauzwa bei gani? R: Itategemea huyo mwenyewe mtengenezaji au huyo mnunuzi kaununua huko kwa bei gani maana muuzaji huwezi ukampangia bei wewe mnunuzi bei anaipanga yeye mwenyewe huko alikonunulia kainunua bei gani ili naye apate chochote akija huku atauza kwa bei anayoitambua yeye I: Wewe huwezi ukakadiria kwa mfano wewe ndiyo unaukuta sokoni unaweza ukasema mimi huu naununua kwa shilingi ngapi? R: Sasa hapo I: Kwa kukadiria tu R: Sababu umekipenda hata ukiambiwa shilingi elfu tano unanunua maana umeupenda na hauna jinsi

chanzo: Amani-Stade Project / Amani Field Research 2023 / Interview No. 04
mwandishi: I: Mohamed Seif, R: Anonymous
Mtu
  • National Institute for Medical Research (NIMR) (Mteja)
  • unknown actor (wissenschaftlicheR BearbeiterIn)
Mahali
  • Amani
Scientific use:
Wakati
2023-06-15
Maelezo
I: na picha nyingine, picha hii imesajiliw kwa namba 2018_18555_001, hebu angalia picha hiyo, unaweza ukatambua hiki ni kitu gani R: huu kwa waswahili wanasema ''mtemba' lakini sisi tunaita 'kiko'... I: kiko ni lugha gani R: ni kisambaa I: na mtemba R: mtemba ni kiswahili ambacho watu wanachukua tumbaku wanaweka kwenye mtemba, basi mtu mwenyewe akiwa kule anavuta I: kwa hiyo kisambaa ni kiko R: kiko ee, mtu anakuambia kaniletee kiko changu, yani kanilete mtemba wangu, halafu na mkaa na uulete ule mkaa vizuri akija anaweka kiko lake hapo, basi yeye mwenyewe amekaa huku kando haswa haswa majumbe ndio wanavuta, akimaliza anakung'uta hata kama ni sehemu ukikaa karibu anaweza akakukung’utia halafu anakuambia nenda ukaondoe hilo jivu lote tena unaanza tena, lakin kwa sasa hivi wanaitengeneza lakini sio kama ya zamani, hii ya zamani iko still sana yaani ni mizuri mno I: ni majumbe tu ndio walikuwa wakivuta R: ni watu maarufu ambao wanavuta, wadoe wanavuta lakini mbele ya jumbe huwezi ukavuta mtemba kama ule, labda nyumbani mwako na wake zako, lakini umekaa na jumbe uvute huo, anakumbia huyu ni nani anayetuiga sisi …oh... Wote: wanacheka R: hasa baba yake yule mkande, baba yake alikuwa 'ushe ni ndai we' yani ‘huyu anayetaka kutuchukua milki ni nani’, huyo, na wewe pia huwezi unaogopa kwenda kubanwa au kwenda kuwekwa sehemu ambayo ni mbaya kwa ajili ya kuvuta mtemba au tunaita kiko I: mitemba ilikuwa inavutwa na watu wa makabila gani hasa R: ni watu wenye nafasi tu I: unaweza ukawatambua kwa makabila yao R: sana sana wasambaa, wambugu, wazigua wanapenda sana mambo ya ufalme ufalme, na wenzetu wazigua unamkuta mtu ana nyumba zaidi ya nne, akikuambia kaniletee mtemba wangu kwenye nyumba ndogo basi ukimkuta hapo amekaa hapo nje amekaa kwenye kiti chake, kuna viti vile ambavyo ni vya magunia, basi mtu amekaa anavuta, ukivuta hiyo ni mtu mmoja marufu sana I: na ni mikoa gani hasa kiko na mitemba ilikuwa ikipatikana R: sana sana tanga ndio inapatikana, lakini sana sana mikoa ya bara na uziguani huko, wazigua wanajua sana mambo ya utamaduni sana, wazigua wanapenda sana utamaduni huo, hata viti hivi ambavyo nimeviona, kuna viti kama vya kupigia ngoma kama ile ya mzee chei ambayo ikipigwa kama kuna jambo la ajali au maradhi inamjulisha basi ile ngoma inalia tu yenyewe 'ndi ndi ndi', basi kwenye mikoa ambayo wanapenda sana huu utamaduni ni uziguani huko na hapa kazita pia ambapo ni Handei, ambapo hapa zamani waliita amani-handei I: na ni wazee wa umri gani walikuwa wakivuta kiko R: ni mpaka uruhusiwe, ukishaoa ndio unaruhusiwa uvute kiko I: kwa hiyo walikuwa ni kuanzia miaka mingapi R: kuanzia… yaani wewe tu unaenda uchungaji ukija unarudi unanyonya kwa mama yako, ni uwe na miaka 30, 35 ndio unapewa, na huyo mke ni wa kupewa uende kwenye nyumba ya fulani ndio ukaoe, na pia ukipewa huu mtemba mpaka uukomboe labda kwa babu yako ndio uuvute I: unaukomboa kwa namna gani R: labda umekwenda kumlimia ungwe au kama umempa hela 5 ndio anakumbia sasa ninakuruhusu tumbaku uvute, lakini huwezi ukavuta kama sasa hivi mtu hajamaliza hata darasa la 4 anavuta, zamani ni mpaka uruhusiwe na babu, sio baba yako ni babu, anajua sasa huyu ana mji wake, ana nyumba yake na familia yake ndio anakuruhusu sasa, lakini sasa hivi... Wote: wanacheka R: ah, ni mambo ya kale, yani haya yananikumbusha mambo ya zamani sana I: wanawake walikuwa wakivuta mitemba R: hamna I: kwa nini R: wanawake walikuwa wanachukua sigara ten cent na magadi anaweka hapa, lakini humkuti mwanamke anavuta I: kwa nini wanawake walikuwa hawavuti mitemba R: wanawake walikuwa kweli walikuwa wanaonelewa sana, yani mwanamke hawezi akapewa uhuru, na sana sana yeye ataambiwa niletee mtembo wangu hapo, niletee kiko changu hapo, kiko karibu na kitanda, na hawezi akagusa na yeye akafanya 'fuu' apulizie mwenyewe avute ndio kinakolea huku, anakuambia sana sana njoo uchukue ukatupe majivu halafu tena uniongezee tumbaku I: kwa hiyo wao walikuwa wakitumikishwa R: walikuwa wakitumikishwa tu, hawezi akaruhusiwa kuvuta I: na kiko kwa sasa vinatumika au unadhani vimepotea havina thamani tena katika jamii R: mimi hilo umenikumbusha nina miaka sio chini ya 50 kukiona hiki, niliokota kiko huku mashambani kama hiki kidogo lakini sasa hivi sijaona, sijui kwenye maduka au wamasai wamasai wanaweza wakatengeneza vitu vya utamaduni, lakini kwa sasa hivi huku hakuna na wala nisikudanganye I: umesema hiyo inaendana na tumbaku na mkaa wa moto, na anayevuta umesema anakuwa kwenye kiti maalum, unaweza kutuambia kiti hiki kinakuwaje R: kuna vile viti kama vya magunia vinajikunja vyenyewe, anakunjua halafu anakaa, analala ni kama kitanda lakini sio kitanda... I: ni vile viti vya uvivu wanasema R: ee wanasema viti vya uvivu, hapo basi ukimkuta amekaa hapo, kimbia uondoke uende uchungaji atakutuma kiko tu... Wote: wanacheka R: ukishamuona ametoka nje amekaa hapo na fimbo yake lazima atakuambia, 'hei njoo, kalete kiko', na moto labda hauko pale utatafuta hata nyumba nyingine I: na kilikuwa kuna umuhimu gani kwa utamaduni wa watu uliowataja R: ilikuwa ni kama hawa vijana wa sasa hivi wanaovuta sigara, na mimi mwenyewe pia nimevuta sigara, yani ni kama kinaleta hisia kama kufikiri I: ulisema kuwa vijana walikuwa wanaruhusiwa na babu, ilionekana ilikuwa ni muhimu sana kwenye mswala ya kimila au na kiutamaduni, ilikuwa ina umuhimu gani hasa mpaka inafikia hatua kwamba... R: hii huwezi ukavuta kama ni kijana, anajua kwamba huyu bwana tayari ana mke na ameshaozeshwa, na ndio maana unamkuta naye ana kiko, ni ishara ya kusema wewe umekomaa, ni sawa sawa na wenzetu wamasai akiozeshwa mke ni mpaka ameua simba, na sisi mila zetu tunasema huyu jamaa sasa hivi hawezekani, nayo ndio hivyo hivyo... Wote: wanacheka R: umenielewa hapo, wanasema mradi anavuta kiko huyu amekuwa na nyumba unaiweza na mke wako, manake sio siri zamani tulipokuwa sisi hata muende mkaoge na msichana hujui kwamba ni nini ile, sasa hivi we wanajua, kuna siku moja mimi na jamaa yangu tulikuwa tunakunywa chai tunasoma darasa la 4, unashiria hata huyo mke uliyekuwa naye unammudu ndio unavuta kiko, sasa wewe huna shamba, chakula ni cha kuitiwa na baba yako halafu unavuta sigara, mke wako pia anatunzwa na mama yako na baba yako I: mzee [anonymous] hebu tuambie, kiko walikuwa wanatengeneza wakina nani, wa jinsia gani ana umri gani R: wanaotengeneza ni watu wenye umri wa miaka 20 - 25, lakini wewe kijana huwezi ukatengeneza kiko hiki, kwanza utakianzaje, hata hii miti sasa hivi huwezi ukaipata, hii miti ni still, lakini miti ya sasa hivi ukitengeneza kiko ukivuta tu na huu moshi tayari kinaungua, lakini hii miti ni still sana, na huwezi ukaipata I: unaweza ukatauambia ilikuwa inatengenezwa kwa miti gani.... na hiki ni nini, ni chungungu au ni... R: hiki ni chungu, walikuwa wanatengeneza vyungu, kuna udongo fulani ambao ni mgumu sana kwa kweli, hata ukitenegeneza vyungu unapikia, sasa hivi unasonga ugali kwenye sufuria lakini zamani ni kwenye chungu, mahindi sasa hivi si ni kukoboa lakini zamamni lazima ufunde halafu unaloweka, ugali wa wake ni mzuri mno, sasa ni udongo ambao sielewi kama sasa hivi udongo upo I: na huo mti mgumu ulikuwa unaitwaje R: hii miti kwa kweli nimeisahau majina lakini wanasema ni asili kama mpingo lakini kuna kitu wanatoboa kama tundu, wanachoma kwenye moto wanatoboa I: na hiyo kamba R: hii kamba inamsaidia sana sana kwenda kutundika havikai chini I: na hiyo ni kamba gani R: hizi ni kama kamba za katani wanasuka au hii minyaa ambapo hata vitanda wanasuka masupato yale, sasa hivi tuna lala kwenye mbao lakini vitanda vyenyewe ni vya supatu, kwa kweli umenikumbusha mengi sana, hasa hii mambo ya kiko na ile miti ya amani I: na kiko kama hicho sasa hivi kikaletwa, sasa hivi kinaweza kuuzwa kwa shilingi ngapi R: aah, hiki labda laki moja au laki mbili, kwanza nitakitoa wapi, kukipata kwanza sio rahisi

chanzo: Amani-Stade Project / Amani Field Research 2023 / Interview No. 21
mwandishi: I: Mohamed Seif, R: Anonymous
Mtu
  • National Institute for Medical Research (NIMR) (Mteja)
  • unknown actor (wissenschaftlicheR BearbeiterIn)
Mahali
  • Amani
Scientific use:
Wakati
2023-09-09
Maelezo
I: tuende na picha hii, picha hii imesajiliwa kwa namba 2018_18555_001, hebu iangalie hiyo R: Hiki wametumia miti fulani yenye upenyo katikati.......... I: Na hicho ni ‘Kiko’ pia R: Eee ni ‘Kiko’, ni kama huo muanzi kwa sababu una njia, kwa hiyo huku kwa afrika anaweza kutengeneza hiki, lakini mzungu akichukua akifika anakitengeneza zaidi ili kumvutia mwafrika aweze kukinunua, lakini hiki ni cha sisi wenyewe waafrika I: Hicho ni cha waafrika R: Eee kwa sababu hii miti tunayo huku I: ‘Kiko’ kama hicho ulishawahi kukiona R: Eeeh ndio, kwa wazee wa zamani, hiki bibi yangu alikuwa anakiuza I: Hiyo namba mbili R:Bibi yangu alikuwa anavuta hiki anaye mzaa mama, anakipenda sana hiki I: Hicho ni ‘Kiko’ namba mbili R: Eeeh hiki anakipenda sana chenye mrija, akikaa kwenye kochi nyie mnaongea huku yeye anavuta tu, tumbaku anaweka mwenyewe sababau inawasha, huwezi kumwambia mtoto fikicha halafu uweke hapa mtoto atawashwa, lakini wewe mwenyewe ukifikicha saa nyingine unaweza hata kuramba kwa sababu umezoea kuvuta, lakini kwa mtoto ukimwambia weka tumbaku hapa itamuathiri, kwa sababu hiyo nayo ikiingia machoni ni sumu macho yanawasha, ndio sababu hao unakuta macho ni mekundu kwa sababu ya tumbaku I: Na uvutaji huu wa ‘Kiko’ ilikuwa lazima ufundishwe ama mtu anawezaje kuwa mvutaji wa ‘Kiko’ R: Unajua wewe unapovuta kile ‘Kiko’ hata wakwe zako wakikuuliza wewe unawezaje kufanya hivyo, unamuambia kwamba ukibandika hapa wewe kazi yako ni kufanya 'pu pu pu' na wewe unafanya hivyo unakibandika huku unavuta, kwa hiyo akikaa hapa anaona raha sana akiwa anavuta hiki ‘Kiko’, hivi viko vilikuwepo siku nyingi I: Na walikuwa wanavuta wazee peke yake na sio vijana R: Unajua watu wa zamani sio watu wa siku hizi, mtu wa zamani hawezi kumpa mtoto hiki avute, watoto wadogo hawatakiwi wavute hivi, wanasema watoto wadogo wakivuta watapata shida I: Nakumbuka asubuhi ulisema ‘Mtemba’ wake ulikuwa unatumika pia kuponya R: Unajua huu ‘Mtemba’ saa nyingine unakuwa na kitu kama nta huko ndani, nta fulani kwa sababu ya ule moshi wa tumbaku, sasa ile nta saa nyingine kama mtoto amekula san amevimbiwa anapakwa kwenye kitomvu hapa, akishapakwa hapa basi saa zote anatoa hewa na tumbo linapungua I: Nta ya kutoka kwenye ntemba wa ‘Kiko’ R: Anapakwa hapa kwenye kitovu I: Na anapona R: Eeh akikaa kila saa anajambajamba na tumbo linapungua mambo yamekwisha I: Anacheka, ilikuwa ni kwa ajili ya kuvimbiwa tu au ilikuwa inafanya na mambo mengine R: Hapana ni kwa ajili ya kuvimbiwa kama mtoto amepata gesi basi anachukua hii anapakwa hapa, akijamba basi tumbo linapungua I: Mzee [anonymous], hicho namba 2 umesema ndio bibi alikuwa anatumia kama hicho R: Eee I: kuna hicho kingine kirefu kikubwa, kichwa chake ni kikubwa kidogo, unadhani ni kwa nini vilitengenezwa kinu kidogo na vinu vikubwa R: unajua saa nyingine kuna ‘Kiko’ kinachoingia tumbaku nyingi na kinachoingia tumbaku kidogo, hiki kinaingia tumbaku nyingi, kwa nini , atavuta kwa muda mrefu, lakini hiki hatavuta kwa muda mrefu I: hapo uliposema kinachukua muda mrefu, je tumbaku ikiisha halafu inazimwa R: inazimwa ndio, ile tumbaku akishaibandika hapa akiona kama ni kali anaikung'uta sehemu fulani ili izimike yenyewe, maana unajua hii inawaka ikivutwa, kwa hiyo kuna ‘Kiko’ kinachoingia tumbaku kidogo na tumbaku nyingi, unajua mtu mmoja anaweza kuwa na ‘Mtemba’ mmoja lakini una vichwa vingi lakini saizi ni ile ile, kwa hiyo saa nyingine anabailisha kichwa, sio kwamba kila ‘Mtemba’ mpka uwe na ‘Kiko’ chke na kinu chake cha kuvutia I: na ni kipindi gani asa walikuwa wakivuta mitemba, ni muda wowote tu akijisikia au kulikuwa kuna vipindi maalum R: unajua saa nyingine hawa wazee wanatabu, saa nyingine anaweza kuvuta akiwa na njaa, akiumwa na njaa anasema anapunguza njaa, au wakati mwingine kama anataka kuvuta ni kwa kujiburudisha I: kuna sehemu tulipita tukaambiwa kwamba walikuwa wanatumia kuvuta ‘Kiko’ wakiwa na mikutano, wazee wanakaa wanajadili mambo yao ndio basi kinatolewa kila mmoja ana cha kwake wanajadili R: wakati mwingine hiki ‘Kiko’ kinavutwa kukiwa na mkutano au kuna habari ya mtoto ambaye anataka kuoa mnataka mtume mahari, sasa pale kuna wazee wenye busara wanaitwa pale kwa ajili ya kutuma mali, kwa hiyo ukisema juu ya kutuma le lazima avute ili akili ikae sawa sawa, au kama mtoto amekosa anakalishwa chini aonywe, mze lazima avute ili apandishe akili iwe vizuri wote: wanacheka

chanzo: Amani-Stade Project / Mlalo Field Research 2023 / Interview No. 05
mwandishi: I: Mohamed Seif, R: Anonymous
Mtu
  • National Institute for Medical Research (NIMR) (Mteja)
  • unknown actor (wissenschaftlicheR BearbeiterIn)
Mahali
  • Mlalo
Scientific use:
Wakati
2023-09-10
Maelezo
I: Sawasawa naomba hiyo nikupatie picha nyingine hii picha ya pili imesajiliwa kwa namba 2018_18555_001 hebu angalia na hii unaweza ukatuambia ni kitu gani hicho? R: Hiki ni kipunde pia ni aina nyingine ya kipunde wanachoweka mapambo eeh lakini hiki hasa vile nilivozungumza kwamba unaweza kuweka jiwe la moto hiki asili yake ni kuweka jiwe la moto I: Kuweka jiwe la moto? R: Eeeeh na kulipulizia bububuu linalia huku mbele ule moto I: Kwahiyo hiko ni kipunde pia? R: Ni kipunde pia I: Labda unaweza ukatuambia kwa makabila haya uliyoyataja ni kabila gani walikua wanapenda kutumia sana kipunde cha namna hiyo? R: Ni sehemu za wapare I: Wapare? R: Eeeeh wapare I: Ni sehemu za wapare R: Ndiyo I: Wasambaa hawajawahi kutumia? R: Hiki cha hivi hiki hapana cha mti mrefu lakini wasambaa chao ni kifupi hakifiki mbali zaidi ndiyo I: Wapare ndiyo walikuwa wakitumia hivyo vyenye mti mrefu? R: Ndiyo

chanzo: Amani-Stade Project / Mlalo Field Research 2023 / Interview No. 01
mwandishi: I: Mohamed Seif, R: Anonymous
Mtu
  • National Institute for Medical Research (NIMR) (Mteja)
  • unknown actor (wissenschaftlicheR BearbeiterIn)
Mahali
  • Mlalo
Scientific use:
Wakati
2023-09-14
Maelezo
I: Sawasawa ngoja tuchukue picha nyingine saa nina picha nyingine hapa imesajiliwa kwa namba 2018_18555_001, mzee [anonymous] hebu angalia alafu mpe na mzee [anonymous] hapo umeona eeh ni nini hicho? R1: Mimi naona ni hichohicho ‘Kiko’ I: ‘Kiko’ kama hiki mzee [anonymous] ushawahi kukiona, kama unakumbuka kama umekiona hebu tuambie? R1: Nimekiona lakini kwa hizo kamba sijawahi kuona hizo kamba eeh lakini kwa urefu nimekiona I: Labda tukijadili hiki kinachoonekana unaweza ukaona utofauti baina ya hiko kimoja na kingine mzee [anonymous]? R1: Tofauti yake ni hiki cha kuwekea tumbaku hiki ni kirefu na hiki ni kifupi ndiyo utofauti wake pia I: Unadhani kwanini kimoja kiliwekwa kifupi na kingine kirefu mzee [anonymous]hebu tueleze hapo? R1: Mimi nadhani ni mapambo tu mtu ukitaka tu ukipenda kwamba nataka aina hii maana hiki kinaingia tumbaku nyingi na kwasababu mtu havuti mwanzo mpaka mwisho kumaliza anaivuta vuta alafu baadae anaondoa tumbaku alafu baadae atavuta tena na hii hapa inaingia tumbaku chache pengine ndiyo sababu

chanzo: Amani-Stade Project / Mlalo Field Research 2023 / Interview No. 10
mwandishi: I: Mohamed Seif, R1: Anonymous
Mtu
  • National Institute for Medical Research (NIMR) (Mteja)
  • unknown actor (wissenschaftlicheR BearbeiterIn)
Mahali
  • Mlalo
Scientific use:
Wakati
2023-09-14
Maelezo
I: Mzee [anonymous]? R2: Mimi nakiangalia ni ‘Kiko’ hicho ila hapo kuna kamba sijui inaninginizwa wapi ila hicho ni ‘Kiko’ I: Sawasawa mzee [anonymous] hebu tuambie unaweza unaweza ukatambua vitu gani vimetumika hapo kutengenezea hivyo viko viwili? R2: Hapa ‘Kiko’ kama hiki ukilinganisha ni udongo tu wa mfinyanzi ndiyo umetumika katika kutengeneza I: Wa rangi gani huu? R2: Hii rangi nyeusi I: Rangi nyeusi? R2: Ndiyo na huu mti uliotumika ni aina ya miti fulani tunaita mianzi ina njia katikati anauchonga chonga I: Na hii kamba unadhani ilikuwa inatumika kufanya nini R2: Inapatikana hata huku kwetu naweza kwenda kuutafuta sehemu za msituni huko inapatikana yenye njia katikati R2: Hivi viko hivi nimewahi kuviona kwa hao hao wazungu wakati ule wanawaita wadutch kwa kipindi hicho I: Walikuwa wanaitwa wadutch kipindi hiko? R2: Eeeeh wadutch ndiyo unamkuta ameshikilia ‘Kiko’ chake yupo mahali ametulia ndiyo tumeona kama hivi na vya kwao vilikuwa vimeboreshwa kuliko hivi vya mababu zetu wanavyo vuta ndiyo tunashangaa vya kwao kumbe wameboresha zaidi I: Kwahiyo waliboresha zaidi? R2: Eeeeeh I: Sawasawa mzee [anonymous] ‘Kiko’ kama hiki kingeletwa katika hali yetu ya sasa kikakutana na yule mtu anaye vuta unadhani angeweza kununua shilingi ngapi mzee [anonymous] hebu tuambie hapo? R2: Hiki kingeuzwa hata shilingi elfu thelathini kwa kweli maana ‘Kiko’ na ubora wa hali ya juu kwa kweli I: Kwanini? R2: Kwa ubora wake kilivyo boreshwa I: Kilikuwa kina vutwa na wadutch? R2: Wanaojua thamani ya viko kina thamani sana I: Hao wa dutch mlikuwa mnawaona mwaka gani hapa? R2: Hapa mwaka 1963 walikuja 1964, 1965, 1966 hadi 1967 walikuwa wanakuja sana huku kwetu I: Mpaka 1967? R2: Eeeeh

chanzo: Amani-Stade Project / Mlalo Field Research 2023 / Interview No. 10
mwandishi: I: Mohamed Seif, R2: Anonymous
Mtu
  • National Institute for Medical Research (NIMR) (Mteja)
  • unknown actor (wissenschaftlicheR BearbeiterIn)
Mahali
  • Mlalo
Mwandishi: Karl Braun, Tarehe ya kutengenezwa: 1905-11-30, Nukuu/Angalizo: Museum der Kulturen Basel, VI 56197, 46 (41)jifunze zaidi
Mwandishi: Karl Braun, Nukuu/Angalizo: Museen Stade, r 2018 / 18566jifunze zaidi
Mwandishi: Karl Braun, Tarehe ya kutengenezwa: 1905-03-11, Nukuu/Angalizo: Museum der Kulturen Basel, VI 56197, 44 (80)jifunze zaidi
Asili ya data ya kitu
Museen Stade
Leseni
Creative Commons Namensnennung, nicht kommerziell, keine Bearbeitung 4.0jifunze zaidi
Imepitishwa katika lango imewashwa
2025-12-04T15:39:01+01:00

Rekodi zetu za takwimu zinafanyiwa maboresho kila mara. Tafadhali wasiliana nasi ikiwa una maswali au maoni au ikiwa unahitaji taarifa zaidi au nyingine zinazohusu mali hii. Taarifa juu ya ulinzi wa takwimu.
Rudi kwenye utafutaji